ENEO LA MWALO WA MAKATANI KATA YA NKOME LAJAA MAJI

 


Na mwandishi wetu


Eneo la Mwalo wa Makatani Kata ya Nkome Halmashauri ya Wilaya ya Geita limezingirwa na maji ya Ziwa Victoria baada ya Ziwa hilo kufurika tokea tarehe 2 May.


Jitihada za kuwaondoa wananchi katika eneo hilo zinaendelea licha ya changamoto ambazo zinaleta ugumu katika kuwaondoa.


Akizungumza katika eneo maafa hayo yametokea Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita Dkt Alphonce Bagambabyaki ambaye pia ni Mkuu wa Idara ya Kilimo na Uvuvi Halmashauri ya Wilaya ya Geita amewataka wananchi hao kuondoka katika eneo hilo kwani ni hatari kwa afya na usalama wao.


Pamoja na hayo ametoa agizo kwa waliojenga mabanda ya biashara kusogea mbali na eneo la mwalo  huo mara moja ili kuzuia maafa ambayo yanaweza kutokea.


Naye Mtendaji wa Kata ya Nkome Festo Nsalamba amesema aliitisha Mkutano na Wananchi hao mapema leo May 4,2024 na kuwataka kuondoka katika eneo hilo la mwalo maji yalipo furika.


Aidha amesema eneo hilo lina Zaidi ya watu elfu tano ambao wanafika kwa ajili ya Shughuli za biashara.


Kwa upande wake Afisa Afya Glory Kimambo amesema  hali ya kujaa maji katika eneo la mwalo huo ni hatari kwa afya ya wananchi wanaoendelea kutoa na kupata huduma za chakula katika eneo hilo ili kuepukana na magonjwa ya mlipuko kikiwepo Kipindupundu.


Hii ni mara pili kujaa kwa Ziwa hilo katika eneo la Kata ya Nkome tangu mwaka 2021.


Naye mwananchi wa eneo hilo yalipofurika maji ndugu Kababa Makoba amesema wanaomba muda wa kuhama eneo hilo ili kuendelea kutafuta maeneo mengine ya kuishi.

Post a Comment

0 Comments